Sina budi kumpongeza Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, kwa jitihada zake za kukabiliana na ujangili nchini.
Ama kwa hakika, najua kwamba anaumiza kichwa kufanya kila awezalo kuhakikisha ujangili unakwisha au unapungua nchini.
Katika jitihada hizo, hivi karibuni kupitia wizara yake, alitoa bunduki 500 aina ya AK 47, za kivita mahsusi kwa ajili ya kupambana na ujangili pamoja na magari aina ya Landcruiser.
Waziri alisema bunduki hizo pamoja na magari vitapelekwa katika mapori ya hifadhi nchini kwa ajili ya kuwasaidia askari wa wanyama pori kufanya vyema kazi yao.
Hata hivyo vita ya ujangili wa meno ya tembo haina tofauti sana na ile ya dawa za kulevya.
Ni mtandao mpana ambao umejipanga vyema ili kuhakikisha meno ya tembo yanapatikana kwa uhai au umauti. Mtandao huu si wa Watanzania pekee, mtandao huu unahusisha raia wa nchi za nje hasa Bara la Asia. Na wengi wanaokamatwa, ni raia wa Hong Kong na Thailand.
Kwa mfano, ripoti iliyotolewa Juni 2013 na Taasisi ya Ulinzi wa Tembo Tanzania (TEPS), inaeleza Bandari ya Dar es Salaam ni kituo kikuu barani Afrika kinachotumika kusafirisha pembe za tembo kuelekea China, Vietnam, Japan, Ufilipino na Thailand.
Hivyo basi wakati tukiendelea kuleta bunduki za kivita, magari na kuongeza askari, lazima tujue nani anawalea raia wa China wanaokamatwa na pembe za ndovu na wale wanaohusika katika mtandao huu huko China, Vietnam, Ufilipino na Thailand.
Kwa sababu, hakuna mfanyabiashara anayeweza kufanikiwa katika biashara bila kuwa na wateja. Kama wateja wakubwa wa pembe za ndovu na faru ni raia wa Bara la Asia, basi tujue kabisa kiini cha msiba wetu kinaanzia huko.
Wakati huo huo, hatuna budi kuangalia urafiki wetu na nchi hizo hasa China kwani inaelekea ni wa mashaka hasa pale wanapokaribishwa kuwekeza huku wakitumia fursa hizo kutuharibia mustakabali wetu.
Uchunguzi uliowahi kufanywa na gazeti hili uliwahi kugundua kwamba mtandao wa ujangili una watu wake katika Bandari ya Dar es Salaam, ambao hushiriki kuipitisha mizigo ya pembe za tembo bila kugundulika.
Kinachozua maswali, ni kwa nini makontena mengi yanapita katika bandari hizo bila kugundulika, lakini hushikwa katika bandari nyingine kama Vietnam, Thailand, China na Ufilipino?
Kwa mfano, Januari 2009, mzigo mkubwa wa pembe za ndovu uliondoka salama Bandari ya Dar es Salaam, lakini ulikamatwa Machi 5, Vietnam katika Bandari ya Hai Phong.
Wakati huo huo, hebu tujichunguze na sisi wenyewe kuhusu utendaji wetu, usiri, kubebana, kuoneana haya na kile kinachoaminiwa na Watanzania wengi eti demokrasia.
Majangili wengi wanaokamatwa au kujulikana kabisa kuwa wanafanya ujangili huo, husitiriwa na kuonewa haya kwa sababu tu ya majina yao makubwa, vyeo serikalini na wakati mwingine wanaonekana wana umuhimu kwa nafasi zao serikalini.
Mwenendo huu unasababisha ujangili kuendelea kukolea mithili ya moto wa kifuu kwa sababu majangili hayo yanafahamu fika kwamba, hayataweza kufanywa lolote au hata ikitokea akawepo anayejaribu kufanya lolote basi, atapewa kitu kidogo, kama wasemavyo waungwana ‘penye uzia, penyeza rupia.”
Haiwezekani kuumaliza ujangili kwa risasi pekee au kwa maneno kuwa ‘tuna majina 40 ya majangili’ la hasha. Hii haitoshi, kwa serikali yenye ujuzi na ufahamu wa kiintelijensia kama Tanzania. Itakuwa aibu ya karne iwapo tembo na faru watamalizika na kizazi kijacho kikawafahamu wanyama hao kwa picha pekee.
0715-773366